FIKRA NGUMU


NO. 0001
MRISHO S. MBWEMBWE (ABU WARDA)
Blog: academiccharity.blogspot.com
Likomale. blogspot.com
Phone: 0657-942497
E-mail: mrishombwembwe@gmail.com
Utangulizi:

Leo katika uga huu wa FIKRA MPYA napenda kuwaletea makala ambayo itasaidia kuamsha hari, hamasa na fikra chanya kwa kila atakayebahatika kuisoma habari hii. Ni dhana mpya ambayo itaogeza udadisi na mabadiliko chanya kwenye jamii yetu ambayo tunahitaji ibadilike na kusonga mbele siku hadi siku.

DHANA YA MTAJI KATIKA UJASIRIAMALI AU BIASHARA.

Ndugu zangu, natumaini sote tunajua kuwa ukimuuliza mtu kuhusu suala la mtaji au “kwanini unashindwa kufanya biashara au shughuli fulani ya Ujasiriamali?”; ni dhahiri kuwa 90% au zaidi ya watu watakwambia kuwa “Sina Mtaji” ndio maana nashindwa kuanzisha biashara au Ujasiriamali. Na asilimia hiyo ya wanaojibu hivyo huwa wanamaanisha kuwa “HAWANA PESA au HELA”!!! Hii inamaanisha kuwa dhana ya mtaji inaeleweka kwa kiasi kikubwa au watu wengi kuwa ni PESA. Mbaya zaidi, dhana hii imedumaza fikra zetu kwa kiasi kikubwa na kutufanya wengi tubweteke na tushindwe kuchukua maamuzi sahihi.

FIKRA MPYA…………………………….

Ukweli ni kwamba; ingawa pesa ni muhimu katika biashara au ujasiriamali; si kweli kwamba pesa ndio mtaji mkuu!!!!! Pesa inachukua nafasi ya chini katika mtaji kwa kuwa kuna rasilimali (Mitaji) ambazo kama mtu hatokuwa nazo, basi hata awe na pesa kiasi gani- itakuwa ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu! Kwa ufupi, Mitaji na Rasilimali za msingi kabla ya pesa ni:
1.        Akili/Fikra (Mindset)
2.       Nia/Kuchukua maamuzi (Will)
3.       Rasilimali watu/Nguvu (Human Resources)
4.       Matumizi chanya ya Urafiki au Familia (Roundtable Empowerment System-RES)
5.       Ufahamu sahihi (Knowledge)
6.       Uthubutu na kuchukua hatua (Positive Decision)
7.       Pesa/Hela (Money)

·         Kama tuonavyo hapo juu. Pesa imechukua nafasi ya SABA na si ya KWANZA! Hii ndio sababu kuwa Pesa ni muhimu katika biashara au ujasiriamali lakini sio Msingi. Kuna mambo ambayo tunayakosa ndio maana tumebaki kwenye lindi la kusingizia kuwa hatuna mtaji wakati tuna fursa kubwa ya mtaji ambao yunashinda kuutumia. Nia ya FIKRA MPYA si kulaumiana au kushutumiana bali ni kuamshana na kuamsha hisia chanya zenye kuweza kutubeba kutoka hapa tulipo na kutupeleka hatua kadhaa mbele. Katika toleo lijalo (Namba 0002) nitawafafanulia jinsi gani fursa namba 1 hadi 6 hapo juu zinavyoweza kufanya kazi kwa muujiza mkubwa hatua kwa hatua…………………………………………………………………….


Hadi toleo lijalo (Mwenyezi-Mungu Akipenda); Kumbuka FIKRA MPYA- “Fikiri na Tazama kwa Jicho la Tatu.”………………………………………………














 NO. 0002
MRISHO S. MBWEMBWE (ABU WARDA)
Blog: academiccharity.blogspot.com
Likomale. blogspot.com
Phone: 0657-942497

FIKRA MPYA KUHUSU MTAJI NA VYANZO VYA UJASIRIAMALI NA BIASHARA
Habari za weekend ndugu zangu; leo tena tunakutana katika uga huu wa FIKRA MPYA ili kuendelea kushirikishana katika kupeana maarifa kama sehemu ya maendeleo yetu katika jamii. Kama tunakumbuka vyema, wiki iliyopita tulianza kuzungumzia dhana ya mtaji ambayo wengi tunadhani kuwa PESA ndio mtaji mkuu; lakini nilieleza kuwa kuna mambo mengine tangulizi ambayo ni mitaji mikubwa kuliko pesa- naomba twende pamoja ili niyafafanue:

1.      AKILI/FIKRA (MINDSET)
Fikra ndio kitivo kikuu cha utendaji wa mtu. Ujasiriamali huanza na FIKRA na AKILI ya mtu; kwa mfano; mtu anapowaza kuwa ana uwezo wa kufanya jambo fulani la kijasiriamali, basi huo ndio msingi wa Mtaji wake. Hii ni tofauti na yule ambaye kila mnapozungumza kuhusu biashara anakwambia kuwa yeye hawezi na anaamini kuwa kuna watu maalum walioumbwa kwa ajili hiyo.


2.     NIA/KUCHUKUA MAAMUZI/DHAMIRA (WILL)
Dhamira ni msingi wa pili wa ujasiriamali. Dhamira ni mfano wa mtu kuamua kuitumia bunduki aliyonayo ili aweze kulenga na kupiga mnyama. Hivyo, Dhamira ni mtaji muhimu sana katika shughuli ya kimaendeleo.


3.     RASILIMALI WATU/NGUVU (HUMAN RESOURCES)
Mtu au watu ni mtaji muhimu wa kufanikisha shughuli ya ujasiriamali. Mtu mmoja anaweza kuongeza nguvu kwa kumshirikisha ndugu au rafiki mwenye mawazo yanayofanana na yake ili kuanzisha na kuendesha ujasiriamali.


4.    MATUMIZI CHANYA YA URAFIKI AU FAMILIA (ROUNDTABLE EMPOWERMENT SYSTEM- RES)
Dhana hii ni mpya na muhimu sana katika jamii zetu. Dhana hii inaelezea jinsi ya kubadili mazoea yasiyo na “faida” na kuwa mtaji wenye kuleta mabadiliko makubwa sana kwenye maisha yetu! Kwa mfano; ni dhahiri kuwa, marafiki na ndugu huwa tunachangiana kiasi kikubwa cha pesa kwenye shughuli mbalimbali kama vile; Harusi, Send-off, Birthday, Graduation, Kitchen Party, Ngoma, “Beseni” n.k.! Kwa ufupi ndugu zangu; tunaweza kubadilisha au kuboresha mazoea haya kuwa mtaji wa Ujasiriamali mkubwa sana! Vilevile, tunafahamu kuwa watu huchangia kiasi kikubwa cha fedha katika shughuli hizi- hadi kufikia kiasi cha elfu 60 (single) au laki moja (100,000- double)!! Tuchukulie mfano kuwa katika marafiki na ndugu tunaochangiana tunafikia 50 tu; tuamue kuwa tunataka kuanzisha mfumo wa kuwezeshana kimzunguko (Roundtable Empowerment System-RES) ili kila mmoja kati yetu aweze kuanzisha biashara. Pia tuchukulie mfano mdogo kuwa kila baada ya mwenzi mmoja au miwili tunamchangia mwenzetu mmoja shilingi elfu ishirini (20,000/=) tu kutoka kila mmoja wetu; kwa ufupi anayechangiwa atapata shilingi milioni moja (1000, 000/=)! Kwa kanuni za ujasiriamali; kiasi hicho cha pesa ni kikubwa saaana kuwa mtaji- haswa ukiangalia historia ya wajasiriamali wengi duniani ambao walianza na mtaji na biashara ndogo saana! Njia hii ya kuchangiana itazalisha jamii yenye uwezo mkubwa sana wa kusaidiana kwa kuwa na uwezo zaidi
kiuchumi.


5.     UFAHAMU SAHIHI (KNOWLEDGE)
Ufahamu sahihi kuhusu biashara ya kufanya ni mtaji muhimu sana kuliko pesa. Ni vyema tukaanza na kuongea au kuomba ushauri kwawale ambao wameshaanza au kupitia shughuli ambayo unataka kuifanya- hii itasaidia kukupa ufahamu sahihi kabla ya kuanza.

6.    UTHUBUTU NA KUCHUKUA HATUA (POSITIVE DECISION)
Ndugu yangu; baada ya kuwa na yote hapo juu, kinachofuata ni kuchukua hatua ya kuanza shughuli yako ya ujasiriamali. Tukumbuke kuwa; kwenye jamii kuna watu wengi wenye ndoto lakini wanachoshindwa ni kuchukua hatua ya kuanza kutembea kwenye ndoto yake kimatendo. Kutokana na hili; wengi husema-“ Utajiri uko kaburini kwa kuwa wengi wanakufa na ndoto zao”.


7.     PESA/HELA (MONEY)
Naomba tukubaliane kuwa; pesa inashika nafasi ya saba kwa kuwa hata kama mtu ana pesa, pasipo kuwa na mambo yaliyotangulia ni kazi bure. Hii ndio sababu ya watu wengi waliotegemea na kutumia pesa zao kama mtaji na mwisho wakaua biashara zao!

Hadi toleo lijalo (Mwenyezi-Mungu Akipenda); Kumbuka FIKRA MPYA- “Fikiri na Tazama kwa Jicho la Tatu.”………………………………………………

No comments:

Post a Comment